Monday 21 April 2008

Mhe Rais 2: Chenge nje!

Shukurani kwa Mheshimiwa Rais kwa kusikiliza kilio cha wengi. Nilikuwa nimemwandikia hapo chini kumkumbusha, lakini nimeona hahitaji kukumbushwa kwa hili. Kama wapo wengine wa namna hii, ni vizuri wenyewe waanze mapema kujitokeza na kujiondoa madarakani kabla mkono wa wananchi/sheria haujawaibua hadharani.
Hongera sana Mheshimiwa JK. Daima tuko pamoja ktk kuijenga nchi yetu kwa ari mpya, kasi mpya na nguvu mpya!
-mosonga

......................

Chenge abwaga manyanga (SOURCE: Nipashe, 21 Apr 2008. By Waandishi Wetu)
Kwa mujibu wa taarifa fupi iliyotolewa na Ikulu, jijini Dar es Salaam jana usiku na kukaririwa na Shirika la Taifa la Utangazaji (TBC), Bw. Chenge alimwandikia barua ya kujiuzulu Rais Jakaya Kikwete jana. Rais ameridhia uamuzi huo na kusema ni kitendo cha busara hasa katika mazingira yaliyopo hivi sasa.

Kujiuzulu kwa Bw. Chenge, kunafuatia kuhusishwa kwake na kashfa ya kuwa na akiba ya Sh. bilioni 1.2 kwenye akaunti yake katika kisiwa cha Jersey, nchini Uingereza. Tuhuma za Bw. Chenge ziliripotiwa na gazeti la The Guardian la Uingereza la Aprili 12 mwaka huu.

Wakati huo, Bw. Chenge alikuwa katika ziara ya nchini China na India akiwa ameambatana na msafara wa Rais. Aliporejea nchini, alikaririwa akisema kiasi hicho cha fedha ni vijisenti, hali iliyosababisha ghadhabu miongoni mwa wananchi ambao wengi na maskini.

Aidha, vyama vya upinzani vilivyo katika ushirikiano, vilipanga leo kwenda ofisi hiyo kudai jalada linaloonyesha mali zinazomilikiwa na Bw. Chenge.

Bw. Chenge ni mbunge wa Bariadi Magharibi kwa tiketi ya CCM.
Wiki iliyopita, wafuasi wa vyama vya upinzani na wananchi walioguswa, waliahidi kuandamana kupinga Bw. Chenge kuingia bungeni.

No comments: