Tuesday 2 October 2007

Matukio ya Moto Dar!

Jiko la mafuta lateketeza nyumba Dar

02 Oct 2007
By Kiyao Hoza, Jijini

Jiko la mafuta linalodaiwa kuwa la mpangaji mmojawapo wa nyumba ya vyumba sita limelipuka juzi alasiri na kuteketeza nyumba moja pale Keko Machungwa Jijini na kusababisha hasara kubwa iliyotokana na kuteketea kwa kila kilichokuwemo ndani ya nyumba hiyo.

Tukio hilo limetokea jana, mishale ya saa 9:00 alasiri katika eneo la Keko Machungwa Jijini.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Kaimu Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Temeke, Bi. Simbakalila amesema nyumba hiyo ni mali ya Bw. Abubakar Juma , 52.

Bi. Simbakalila akasema nyumba hiyo ilikuwa na idadi ya vyumba sita, ambapo vinne kati ya hivyo vilikuwa na wapangaji.

Chanzo cha moto huo inasadikiwa kuwa ni jiko la mafuta lililokuwa likitumiwa na mpangaji aliyefahamika kwa jina la Ijumaa Hassan.

Amesema jiko hilo baada ya kulipuka moto ulisambaa na kushika kwenye vyumba vingine.

Hata hivyo thamani ya mali iliyoteketea haijafahamika na imeelezwa kuwa hakuna madhara zaidi kwa binadamu.

Moto huo ulizimwa na Kikosi cha Zimamoto cha Jiji kwa kushirikiana na wakazi wa eneo hilo.
* SOURCE: Alasiri

Moto wateketeza mali ya mamilioni dukani Dar
02 Oct 2007
By Kiyao Hoza, Polisi Kati

Moto umezuka ghafla kwenye kontena moja lililokuwa likitumiwa kama duka na kuteketeza mali yote iliyokuwamo ambayo thamani yake inadhaniwa kuwa ni ya mamilioni ya pesa.

Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi, Kinondoni Jamal Rwambow, ameliambia Alasiri leo kuwa tukio hilo limetokea jana majira ya saa 1:45 asubuhi huko Mbezi Beach, eneo la Samaki Jijni Dar es Salaam.

Amesema kontena hilo lililokuwa linamilikiwa na Bw. Cathbeth Lyimo, 32, mkazi wa Mbezi Juu Jijini Dar.
Kamanda amesema kuwa chanzo cha moto huo kinasadikiwa kuwa ni hitilafu ya umeme.

Amesema kuwa moto huo ulizimwa na Kikosi cha zimamoto cha Halmashauri ya Jiji na hakuna madhara zaidi kwa binadamu.

Wakati huo huo, watu 11 wanashikuliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma kwa kukutwa na Pombe haramu aina ya gongo lita15.

Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Temeke,Emmanuel Kandhabi amesema kuwa watu hao walikamatwa jana majira ya saa 6:00 mchana huko Mbagala Charambe Maji Matitu Jijini Dar es Salaam.

Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Issa Salum,46, Yakob Mussa, 25, Mwanahawa Athuman,45 na wengine nane.

Amesema watuhumiwa watafikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa kijubu tuhuma hizo.
* SOURCE: Alasiri

No comments: