Friday 7 November 2008

EPA: watuhumiwa wafikishwa mahakamani

Watuhumiwa wa kashfa ya EPA wameafikishwa mahakamani wiki hii na sserikali kujibu tuhuma dhidi yao.

1 comment:

MOSONGA RAPHAEL said...

Watuhumiwa wapya wa EPA wafikishwa kortini

2008-11-07 10:21:16
Na Joseph Mwendapole


Watuhumiwa wengine watatu wa ufisadi wa fedha katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashitaka ya kula na mashitaka ya kula njama, kughushi na kujipatia fedha kwa njia ya wizi kiasi cha Sh. bilioni 10.8.

Aidha, washtakiwa wengine 10 waliosomewa mashtaka yao juzi, jana walirudishwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.

Washtakiwa waliosomewa mashitaka jana wanafanya idadi ya watuhumiwa wa wizi wa fedha ndani ya BoT kufikia 13.

Waliosomewa mashitaka yao jana ni Farijala Shaban Maranda, Rajabu Shaban Hussein na Japhet Lema.

Katika kesi ya kwanza, Wakili wa serikali Mkuu, Boniface Stanslaus, aliwasomea mashitaka yao washtakiwa Maranda na Hussein kuwa kati ya Januari 18 na Novemba 3 mwaka 2005, jijini Dar es Salaam, walikula njama za kuiba fedha BoT.

Kesi hiyo ilikuwa ikisikilizwa na Hakimu Mkazi, Warialwande Lema.

Katika shtaka la pili, alisema washtakiwa hao walighushi hati za kuhamisha mali kwa jina la kampuni ya Mwibare Farm ya Tanzania na Lakshmi Textile Mills Ltd ya Mumbai.

Katika shtaka la tatu, Wakili alidai kuwa washtakiwa hao waliiba Sh. 3,868,805,737.13, mali ya BoT.

Pia washtakiwa hao wanashtakiwa kwa kujipatia ingizo la fedha hizo baada ya kudanganya kwamba Kampuni hiyo ya Lakshmi imehamishia deni hilo kwenye akaunti ya kampuni ya Mwibare Farm.

Washtakiwa hao walikana mashitaka yanayowakabili na walitakiwa kuwa na wadhamini wawili.

Hakimu alidai washtakiwa wote hao wawili watatoa nusu ya fedha wanazodaiwa kama dhamana. Fedha hizo zinatakiwa kuwasilishwa taslimu mahakamani.

Washtakiwa walishindwa kutimiza masharti ya dhamana na wamepelekwa rumande hadi Novemba 14 mwaka huu watakaposomewa maelezo ya awali.

Katika kesi nyingine, mshtakiwa Maranda alisomewa mashitaka mengine ya kugushi, kuwasilisha na kujipatia kwa njia ya wizi Sh. 207, 284, 391.44 mali ya BoT kwa kupitia kampuni ya Rashhas ya Tanzania na General Marketing ya nje ya nchi.

Katika kesi nyingine, washtakiwa hao wawili, Maranda na Hussein walisomewa mashtaka yao mbele ya Hakimu Mkazi Nyigulila Mwaseba.

Washtakiwa walidaiwa kuwa waligushi na kujipatia kwa njia ya wizi ingizo la Sh. 2,2666,049,041.65.

Washtakiwa walikana mashitaka yao na walitakiwa wawe na wadhamini wawili ambao ni wafanyakazi wa serikali na watoe fedha taslim shilingi bilioni 1.2.

Katika kesi nyingine, mshtakiwa Japhet Lema mkazi wa Arusha alisomewa mashitaka mawili ya wizi na kujipatia ingizo la fedha kwenye akaunti yake kwa njia ya udanganyifu.

Ilidaiwa kuwa mshtakiwa huyo alijipatia Sh. 2,600,000,000 kupitia kampuni ya Njake Enterprises kwa njia ya udanganyifu akidai kuwa kampuni hiyo imepasiwa deni hilo na kampuni ya C. Itoh ya Japan.

Akitoa masharti ya dhamana, hakimu alisema mshtakiwa huyo haruhusiwi kutoka nje ya mkoa wa Dar es Salaam bila kuwa na kibali cha mahakama, wadhamini wawili wa kuaminika na kila mmoja atasaini hati ya dhamana ya Sh milioni 650 na mshtakiwa anatakiwa kuwasilisha hati ya kusafiria.

Mshitakiwa pia alitakiwa atoe fedha taslimu Sh biloni 1.3 kama dhamana ikiwa ni nusu ya kiasi cha fedha anachodaiwa kuiba.

Hussein na Maranda wanadaiwa kula njama, kughushi, wizi na kujipatia ingizo la fedha kwa njia udanganyifu.

Ilidaiwa kuwa washtakiwa hao mwaka 2005, walijipatia 1,864,949,294.45 baada ya kudanganya kuwa kampuni ya Kiloloma & Brothers ya Tanzania imehamishiwa deni na kampuni ya B. Cars Export Ltd ya Mumbai na hivyo kujipatia fedha hizo.

Washtakiwa walikana mashitaka na kesi hiyo inakuja leo kwa ajili ya dhamana dhidi ya washtakiwa hao.

Baada ya kesi hizo kuahirishwa, ndugu, jamaa na marafiki waliangua vilio nje ya mahakama hiyo baada ya kuwaona ndugu zao wakiingia kwenye magari ya magereza tayari kwa kurudishwa mahabusu.

Ndugu hao walijipanga kwenye misururu nyuma ya mahakama hiyo na kisha kuwapungia mikono huku wengine wakiangua kilio.

Chumba namba moja cha mahakama hiyo, ambako kesi hizo zilikuwa zikisikilizwa, jana kilifurika idadi kubwa ya watu kusikiliza kesi hiyo.

Chumba hicho ambacho hakina vipoza hewa kilizidiwa na idadi ya watu hivyo kuwa na joto kali, hali iliyowafanya watu watumie karatasi na vitambaa vya kujifutia jasho kipepea.

Wakati huo huo, washtakiwa tisa waliofikishwa mahakamani hapo jana kwa tuhuma za kuiibia BoT, Sh. bilioni 31, walishindwa kutimiza masharti ya dhamana na kurejeshwa gereza la Keko.

Hata hivyo, washtakiwa hao pia watarudishwa mahakamani leo na kama watatimiza masharti ya dhamana wanaweza kuwa nje.

Washtakiwa hao ni Jayantkumar maarufu a.k.a Jeetu Patel, Ketan Chohan na Amit Nandy, ambao waligushi na kujipatia Sh. 3,323,974,942.30.

Wanadaiwa kujipatia ingizo la fedha kupitia kampuni ya Navy Cut Tobacco Tanzania Ltd na Mashtushita Electrical Co. Ltd ya Japan.
Katika kesi nyingine, Jeetu Pate, Devendra Patel na Amit Nandy, wanadaiwa kujipatia Sh bilioni 10.

Wanadaiwa kujipatia ingizo la fedha hizo kupitia kampuni ya Bencon International Ltd na Mashtushita ya Japan.

Katika kesi nyingine pia washtakiwa hao walidaiwa kujipatia ingizo la Sh bilioni 4.9 kupitia kampunji ya Maltan Mining Ltd ya Tanzania na Marubeni Corperation ya Japan.

Katika kesi nyingine washtakiwa Bahati Mahenge, Manase Mwakale, Davies Kamungu, Godfrey Mosha na Eddah Nkoma Mwakale, wanadaiwa kujipatia Sh bilioni 2 kwa kutumia kampuni ya Changanyikeni Residential Complex Ltd ya Tanzania kwa niaba ya Marubeni Co-operation ya Japan.

SOURCE: Nipashe