Saturday 21 July 2007

Dar: Nauli za mabasi, daladala zapanda

Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Nchi Kavu na Majini (SUMATRA) imeridhia kupanda kwa nauli za mabasi ya endayo mikoani na daladala kwa asilimia 20. Hayo yalibainika jana wakati Mkurugenzi wa SUMATRABw. Israeli Sekirasa alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es es Salaam juu ya nauli hizo mpya. Mkurugenzi huyo alitaja baadhi ya nauli mpya za mikoani. Kama vile kutoka Tanga hadi Dar es Salaam kuwa ni Sh.7,500 badala ya Sh. 6,500, Tanga hadi Moshi Sh. 8,500 badala ya Sh.7,500. Kuhusu nauli za daladala mkurugenzi huyo alisema kuwa hazitakiwi kuongezeka zaidi ya Sh. 50. ``Kulingana na nauli za awali wanapaswa kuongeza sio zaidi ya Sh. 50. Mfano kama nauli ilikuwa Sh. 200, nauli mpya inapaswa kuwa Sh. 250, au kama ili kuwa Sh. 250 basi inakuwa Sh. 300 na sio vinginevyo,`` alisema. Kuhusu nauli ya mwanafunzi Bw. Sekirasa alisema kuwa itabakia pale pale Sh. 50 hadi kutakapotolewa mapendekezo mengine. Aidha aliongeza kuwa askari na wanajeshi wataendele kusafiri bure kama ilivyo kuwa awali hadi suala lao litakapofikiriwa vinginevyo. ``Mapendekezo tuliyoletewa na watu wa daladala walitaka nauli ya mwanafunzi ipande hadi Sh.100 na wanajeshi pamoja na askari waanze kulipa nauli kama abiria wengine.... Sisi tukawaambia kuwa hilo la wanafunzi libakie hivyo hivyo na hilo la askari na wanajeshi sio vyema tukalijadili hadharani, ila tutaangalia utaratibu mwingine wa kiutawala zaidi ili kupata jibu,`` alisema.
SOURCE: Nipashe, 2007-07-21 10:19:24 Na Godfrey Monyo

No comments: