Friday 17 October 2008

Hongera Majira, Bus. Times (T) Ltd

Nimeona shamrashamra za magazeti ya Business Times Ltd kusherekea miaka 20 tangu kuzaliwa. Mimi kitu ninachombuka sana ni kuwa nakala za Majira zilianza kuuzwa kwa sh. 30/= enzi hizo ikiwa ni bei nafuu kuliko magezi yote kipindi hicho. Magazeti mengi yalikuwa na bei za 50/= au 70/=.

Hongera sana Majira.

1 comment:

MOSONGA RAPHAEL said...

Makala:
Wasifu wa Gazeti la Majira

DESEMBA 27, 1993 gazeti la kila siku la binafsi la Kiswahili lilizaliwa kwa jina la Majira, likiwa ni gazeti dada la Business Times ambalo ni la Kiingereza linalotoka kila siku ya Ijumaa.

Majira ilianza likiwa ni gazeti huru kwa lengo la kuhakikisha kuwa linakuwa ni sauti ya wanyonge lisilo na itikadi yoyote ya kisiasa, likishindana na gazeti pekee la kila siku la Kiswahili la Uhuru linalomilikiwa na Chama Tawala cha CCM.

Ni gazeti ambalo linaandika habari zinazohusu maisha ya kawaida; uchumi; siasa; jamii; sayansi, teknolojia, mazingira na elimu na utamaduni na michezo, huku toleo la Jumapili likiandika habari za kifamilia zaidi.

Lilianza likiwa na kurasa 16 likianza na waandishi waliokuwa na makao yao Dar es Salaam, lakini lilipoanza kujizolea wasomaji wengi likalazimika kuongeza kurasa hadi 20 na wakati mwingine kuzidi hapo kwa kuzingatia wingi wa matangazo.

Hivi sasa Majira ina waandishi karibu kila kona ya nchi huku likiwa na kurasa nyingi zaidi kutokana na kuongezeka kwa matangazo na kuwa miongoni mwa magazeti machache nchini yanayobeba matangazo mengi.

Kuanzishwa kwa Majira kuliibua changamoto kubwa kwa Watanzania ambao walizoea kusoma habari zilizokuwa zikisifia viongozi wa Chama (CCM) na Serikali yake, ambayo sasa iliwalazimisha kuona upande mwingine wa sarafu.

Huo ulikuwa ni upande uliozingatia kueleszea kero za wananchi lakini iliochelea kuishambulia Serikali na CCM, kwa kuamini katika dhima ya taaluma ya uandishi wa habari.

Hata hivyo, Majira haikuchelea kukikosoa chama hicho tawala na Serikali yake, huku pia ikijaribu kuibua fikra za mageuzi nchini kwa kukaribisha pia habari za vyama vya upinzani.

Hatua hiyo ililenga si kuvikumbatia vyama hivyo, bali kuhakikisha kuwa habari zao zinawafikia wananchi kwa kuzingatia taaluma na wajibu wa vyombo vya habari wa kuhabarisha, kuburudisha na kuelimisha.

Gazeti la Majira lilianza chini ya uongozi wa mwanataaluma, Bw. Kassim Mpenda, akiwa Mhariri Mkuu wake wa kwanza, ambaye mchango wake uliotukuka ndio uliofungua njia ya kupita na kufikia mafanikio lililonayo.

Hata hivyo Bw. Mpenda hakudumu sana na Majira kabla ya kurejea serikalini na kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO, nafasi aliyoshikilia hadi kustaafu hivi karibuni.

Wahariri wengine wakuu waliowahi kuliongoza Majira kwa kipindi hiki cha miaka 20 ni pamoja na Bw. Sam Makila, Bw. Anthony Ngaiza, Bw. Theophil Makunga, Bw. Masoud Sanani, Bw. Mobhare Matinyi na sasa Bw. Joseph Kulangwa.

Majira imekuwa ikipitia vipindi tofauti ikikabiliwa na ushindani mkubwa uliotokana na kuanzishwa kwa magazeti mengi ya Kiswahili ya kila siku na hivyo kunyang'anyana wasomaji wachache waliopo.

Pamoja na hali hiyo, lakini pia Majira iliwahi kukumbwa na matatizo ya kufungiwa kuingia Zanzibar na kufungiwa siku saba na Serikali ya Jamhuri ya Muungano kutokana na sababu za kitaaluma.

Kwa kipindi chote hicho katika muktadha wa kunyang'anyana watendaji, Majira iliwahi kuondokewa na idadi kubwa ya waandishi wa habari kwenda kuanzisha magazeti kama Leo ni Leo pamoja na Mwananchi.

Lakini pia imechangia katika kuwa na waandishi wengi katika vyumba vya habari vingi nchini kulikotokana na wenye kampuni za vyombo vya habari kuchukua waandishi wengi kutoka Majira.

Hata hivyo pamoja na kuporwa waandishi, Majira imejiimarisha na sasa inatarajia kukua zaidi na kujitanua hata kuwa gazeti kiongozi si tu nchini bali Afrika Mashariki.