Tuesday 27 May 2008

'Nyumba ndogo' hualikwa na 'kubwa'?

* SOURCE: Nipashe, 25 May 2008.
By Anti Flora Wingia (e-mail: fwingia@yahoo.com)
Nina mfano mmoja ni wa kweli kabisa na bwana huyo kila siku amekuwa akilalamika juu ya hilo akitamani hata kujinyonga.

Ndugu huyo ni mfanyakazi katika kampuni fulani, kila miezi sita huwa porini, arudipo mjini hupata kiwango kingi cha pesa kulinganisha na mshahara mdogo wa kila mwezi.

Msimu wa mwaka 2005 aliweza kununua sehemu ya kuweka banda la kusetiri familia yake akitegemea msimu ujao ataanza hata ujenzi.

Msimu wa 2006 alitegemea kujenga lakini mafao hayakuwa mazuri, ila aliona anunue bati kadhaa kwa kuwa haziozi ili zimsaidie muda wa ujenzi utakapo wadia.

Wakati anasubiri msimu wa 2007, mke kauza zile bati kisirisiri na pesa hizo hatujui kazifanyia nini. Mwisho wa msimu huo huo tena kaamua kuuza kile kiwanja na kusakafia tena pesa zake.

Mume aliporudi hana bati wala kiwanja. Kwa kweli alichanganyikiwa na sasa ameamua kuwa mlevi. Je huyo bwana akipata kimwana cha kumliwaza huyo bibie hajaachwa kwenye kichumba chake cha kupanga?

Jamani hata sisi kinamama tunatakiwa tuwe mstari wa mbele kusaidiana na waume zetu kwa namna moja au nyingine.

Kweli wako wenye bidii na nina hakika waume zao wanawaheshimu na kama ni kuiba hata sisi kina mama twaiba lakini kwa akili...ila kazi kwetu jamani VVU.

....................................
Msomaji mwingine anasema ifuatavyo:-
Napenda kuchukua nafasi hii kotowa shukrani zangu kutokana na maoni yako kuhusu matatizo yanayotukabili sisi wanaume kuoa mabibi wawili.

Ukweli ni kuwa ni vigumu sana mwanamume kuwatosheleza kimapenzi wake wawili, ni lazima wote watatembea nje hasa wakijua ya kuwa mume wao ana nyumba mbili.

Nimeshuhudia mimi binafsi wanaume wanavyopata maradhi ya moyo au blood pressure kutokana na hao wake wawili.

Bwana anapokwenda kwa bibi mkubwa na kutaka chakula anapigiwa kelele na kutukanwa na kuambiwa aende kwa yule bibi mdogo, hali kadhalika akienda kwa bibi mdogo matatizo ni yale yale kutukanwa na kusimangwa.

Balaa yote hiyo ni sisi wanaume tunajitakia kwani kurithisha mabibi wawili ni kazi kubwa sisi wanaume hatuwezi, kwani mshika njia mbili moja humponyoka. Anahitimisha maoni yake msomaji wetu huyu.

No comments: