Wednesday 1 August 2007

Michuzi atapeliwa!

Tuesday, July 31, 2007

Mahojiano na Kaka Michuzi juu ya site yake kuwa Hacked!

KUTOKA BONGO CELEBRITY.com
Yawezekana umeshapata ujumbe uliosambazwa na Issa Michuzi mwenyewe au ule ambao Da’Chemi wa Swahili Times blog ameusambaza ikiwa ni tahadhari kuhusu e-mail ya kitapeli ambayo ilisambaa jana na bado inaendelea kusambaa hivi sasa ikidai Issa Michuzi amekwama hotelini huko nchini Nigeria na hivyo anaomba msaada wa kifedha.
Tungeweza kuipuuzia tu e-mail kama hiyo.Tatizo ni kwamba sio tu ni ya kitapeli,bali hivi sasa imemfanya Issa Michuzi ashindwe hata ku-update blog yake maarufu. Kimsingi e-mail ya issamichuzi at gmail ambayo ndio aliyokuwa akiitumia kuingia ndani ya blog yake haipo mikononi mwake tena! Ndio maana kama mnavyoweza kuona ukiitembelea blog yake tangu jana hajaweza kuweka picha mpya,jambo ambalo sio kawaida yake kabisa.
BongoCelebrity imewasiliana na Michuzi na kufanya naye mahojiano yafuatayo. Yasome na kisha mkumbushe na mwenzio kuhusu kwamba aipuuzie tu e-mail kama hiyo. Hapa Michuzi anaelezea nini kilitokea,lini ataweza tena kuendelea ku-update blog yake(archives zote bado zipo na zinapatikana online),vipi unaweza kuepuka yasikukute yaliyomkuta na anapatikana kwa njia gani hivi sasa? Majibu haya hapa chini;
BC:Nini hasa kimetokea? Ilikuwaje?
MICHUZI: Jana mnamo saa tatu na robo usiku nilifungua mtandao nyumbani na kupost picha kama nane hivi, ikiwa ni pamoja na za Rais mstaafu wa Marekani Bill Clinton na kumalizia na ya mafuvu ya wahanga wa mauaji ya kimbari kule Rwanda ambayo kuna mdau alinitumia. Kisha kama kawaida nikaingia kwenye issamichuzi at gmail.com ili kupitia maoni kama kawaida kwani issamichuzi.blogspot.com nimeitegesha kwamba maoni hayaendi moja kwa moja bali yanapita kwanza kwenye email yangu ndipo kama naona yanafaa nayaruhusu na kama hayafai nayazuia. Basi bwana, kwenye saa tano kasorobo hivi, ukaingia ujumbe ukidai unatoka kwa ‘Gmail Team’ unaofanya censor kutokana na malalamiko kwamba gmail siku hizi bomu kwa kuwa watu wamekuwa wengi, hivyo ujumbe ukanieleza jaza details zako ndani ya siku saba kama hutaki account yako kufutwa toka gmail.
Siku ya kufa nyani miti yote huteleza. Na mimi ujumbe kama huo sio mara ya kwanza lakini wa safari hii, kama ningekuwa naamini juju-nangai ningesema jamaa wamepulizia maana nikajikuta najaza jina langu, umri na hata password na kusend. Huo ndio ukawa mwisho wa issamichuzi at gmail.com kwani nusu saa baadaye nikawa siwezi kuingia kwenye gmail tena.
BC:Uligundua vipi na saa ngapi kwamba e-mail yako imekuwa hacked?
MICHUZI: Niligundua niko hacked kwenye saa sita kasoro kumi wakati Da’Chemi aliponipigia kutoka Marekani na kuniuliza nimeenda lini Nigeria naye alipoondoka aliniacha Dar? Nikajua nimeshaumia baada ya kunieleza kwamba kuna mtu kaiba email yangu ya Gmail na anasambaza ujumbe wa kuomba msaada wa pesa kila mahali. Tukaingia kazini mimi na Chemi kuanza kuarifu watu wote tulioweza kuwafikia. Yeye kupitia blog yake ya Swahili Times nami kwa simu ya mkono na email yangu ya yahoo. Kwa kweli imenisaidia sana la sivyo saa hizi tungekuwa tunaongea mengine kwani wengi wangeamini ni mimi na kutaka kutuma pesa. Tena jamaa walivyokuwa hawana haya ati wamendikia hata mimi mwenyewe kupitia anuani yangu ya yahoo kuomba msaada wa pesa. Hahahaaaa!
BC: Umejifunza nini kutokana na tukio hili? Unawaambia nini wanablog wengine ili wajihadhari na tukio kama hili?
MICHUZI: Nimejifunza mengi sana, lakini kubwa na ambalo limenigusa sana moyoni ni kwamba wadau wananithamini na hakuna aliyesita kuniunga mkono na kuweka wazi kuwa tupo pamoja katika wakati huu mgumu.
La pili nililojifunza ni kwamba mtu usi-panic kwenye aina yoyote ya emergency, keep cool and ponder each and everything in its own perspective otherwise you will compromise your judgement the way your email address has. Usikurupuke.
Tatu na mwisho ni kuhakikisha una plan B katika kila ufanyacho kwenye maisha, hata kama yamekunyookea vipi. Kwa lugha nyingine hata kama blog itakufa leo (na haifi) nina plan B ambayo ni kubwa pengine kuliko blog.
BC: Unawaambia nini wadau wako.Lini site itarudi hewani?
MICHUZI: Asante kwa swali hili kwani wengi wametafsiri kwamba mtandao wa Michuzi ume-kuwa hacked na umekufa ama hauko hewani. Ukweli mtandao haujaguswa na wala hao jamaa hawajaingia huko. Wao wameingia kwenye email yangu ya Gmail na kuiba password kwa nia ya kutapeli watu. Uzuri wabongo sio mazezeta kama hawa jamaa wa ki-Nigeria wanavyodhani. Hivyo kukujibu lini narudi hewani ni kwamba kwa muda mfupi nitaacha ku-posti picha kwani ni hadi google watakaponipa password mpya pamoja ndipo nitaanza tena. Lakini kama unavyoona ukisearch issamichuzi.blogspot.com ama uki-google ‘michuzi’ unaipata blog yako kama kawaida kwani bado iko hewani.
BC: Unawaambia nini wadau,ndugu, jamaa na marafiki ambao walikuwa kwenye e-mail list yako? Wachukue tahadhari gani?
MICHUZI: nawaambia waachane kabisa kabisa na issamichuzi at gmail.com na watumie jina hilo hilo katika yahoo.com
BC: Wanaotaka kuwasiliana nawe hivi sasa watumie njia gani?
MICHUZI: issamichuzi at yahoo.comKama bado hujaisoma e-mail yenyewe ya kitapeli unaweza kuisoma pale Swahili Times.Developing story…Michuzi hivi sasa anapatikana katika http://isamichuzi.blogspot.com/Tofauti yake na ile blog ya zamani ni “s” iliyopo kwenye issa,badala ya s mbili weka moja.
Labels: , ,
posted by Chemi Che-Mponda at 11:07 AM 0 comments

source: swahili time blog (Chemi Che Mponda-Kadete)

No comments: