Tuesday 8 July 2008

Unyumba ruksa lupango

(source: majira, Na Nicodemus Ikonko, Hirondelle, Arusha. 05.07.2008 0143 EAT)
Wafungwa, mahabusu ICTR sasa ruksa kujamiiana gerezani

MAHAKAMA ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) imebadilisha sera zake kwa kuruhusu watuhumiwa na wafungwa wa mahakama hiyo, kujamiiana.

Hiyo ni sehemu ya juhudi za kuoanisha sheria za ICTR na mahakama nyingine za Umoja wa Mataifa za Uhalifu wa Kivita katika Yugoslavia ya zamani (ICTY).

Kuanzia Mei mwaka huu, sera mpya inayoruhusu kujamiiana imekubaliwa na ofisi ya Msajili ili kuoanisha sera za ICTR na zile za ICTY,” alieleza jana Msemaji wa Mahakama hiyo, Bw. Roland Amoussouga.

Alisema haki ya kujamiiana ya watuhumiwa na wafungwa na wapenzi wao, itatolewa kwa kufuata taratibu maalumu zilizowekwa katika sheria inayohusu kuwekwa kizuizini na hatua yoyote ya kukiuka utaratibu huo, itamnyima mhusika kupewa tena nafasi kama hiyo.

ICTR hivi sasa ina jumla ya watuhumiwa 56 katika gereza lake maalumu mjini hapa pamoja na wafungwa 18 ambao wanasubiri kupelekwa katika nchi mbalimbali zilizokubaliwa kwenda kutumikia adhabu zao.

Utaratibu huo wa aina yake, ulikuwa unafanyiwa kazi tangu mahakama hii imkatalie haki ya kutaka kuoa, mfungwa mmoja, Bw. Hassan Ngeze, Mhariri wa zamani wa gazeti la Kangura la Rwanda mwaka 2005, hatua ambayo ingemruhusu kutembelewa na mkewe mtarajiwa kwa madhumuni ya kujamiiana.

Bw. Ngeze anatumikia kifungo cha maisha jela baada ya kutiwa hatiani kwa mauaji ya kimbari na uchochezi.

“Watuhumiwa huchukuliwa kuwa hawana hatia hadi inapothibitishwa vinginevyo na mahakama, na wafungwa wanatakiwa kunyimwa haki yao ya kwenda huru wanakotaka na si vinginevyo,” alifafanua Bw. Amossouga.

Alisema suala hili halijakubaliwa mahala pengi duniani na kuongeza, kwamba Mahakama ya Umoja wa Mataifa ina jukumu la kusambaza baadhi ya haki za msingi za watuhumiwa na wafungwa.

Kwa mujibu wa ICTR, mgeni atakayewatembelea watuhumiwa au wafungwa husika kwa lengo hilo la kujamiiana, pamoja na mambo mengine, anaweza kukaguliwa kwanza taarifa zake, na mfungwa au mtuhumiwa husika lazima awe hana magonjwa ya zinaa.

Wahusika hao wa pande zote mbili pia kama sehemu ya utaratibu, lazima wakaguliwe kabla ya kuingia na kutoka gerezani ili kuhakikisha kwamba mgeni haingizi vitu visivyotakiwa ndani au kutoka navyo nje ya gereza.

Ruhusa za kutembelea wafungwa na watuhumiwa kwa ajili ya kujamiiana, hutolewa kwa muda wa juu kabisa wa saa tatu na hairuhusiwi kusumbua majirani.

Kwa mujibu wa chanzo cha habari cha Shirika la Habari la Hirondelle, hakuna mfungwa au mtuhumiwa atakayeruhusiwa kutembelewa kwa minajili hiyo zaidi ya mara moja katika kipindi cha miezi miwili mfululizo, isipokuwa kwa watuhumiwa ambao wapenzi wao wanaishi katika nchi mbali na Tanzania.

Hata hivyo, katika mazingira kama hayo, mgeni mhusika ataruhusiwa mara moja kujamiiana na mpenzi wake katika wiki ya kwanza na mara ya pili katika wiki ya mwisho ya wanafamilia kutembelea wafungwa au watuhumiwa.

Suala la wafungwa au watuhumiwa kupewa haki ya kujamiiana bado linaendelea kuleta majadiliano makali duniani, huku baadhi ya nchi zikisisitiza, kwamba watu wa aina hiyo wasipewe haki hiyo hata kama anayetaka kujamiiana naye ni mke au mumewe kutokana na dhana, kwamba kunyimwa haki hiyo ni sehemu ya adhabu.
......................................................................

Maoni yangu: wafungwa na mahabusu wapewe haki kujamiiana na wenzi wao! Kifo tu ndo kitawanyang'anya hiyo haki!
.......................................................................

1 comment:

MOSONGA RAPHAEL said...

Mmh! Hili sasa ni 'so' kutoka serikali ya Rwanda! Nini kinawauma hawa jamaa? Mtu na mke au mume wake (au hata kama ni girlfriend/boyfriend wake?) kuna tatizo gani hapo jamani?

Mtu yuko gerezani hana uhuru wa kwenda popote -hiyo ni adhabu tosha- sasa kwanini na wenzi wao nao wapewe adhabu ya kukosa unyumba na kuongeza familia (kuzaa)?

Makosa ya mfungwa yasibebeshwe kwa wenzi wao tafadhalini wangwana eee!!!!

...........................
...........................
(Source: Majira, 08.07.2008 0032 EAT. Na Mwandishi wa Hirondelle, Arusha)
Rwanda yapinga wafungwa kujamiiana magerezani
SERIKALI ya Rwanda imepinga sera mpya ya Mahakama ya Kimataifa ya Kesi za Mauaji ya Kimbari nchini humo mwaka 1994 iliyoko jijini hapa(ICTR), ya kuruhusu watuhumiwa na wafungwa kujamiiana gerezani kuwa inakejeli na kukiuka sheria.

"Watu wengi nchini Rwanda wanaiona sera hii ya ajabu ... sijui Mahakama hii inataka kuacha kumbukumbu gani," alisema Bw. Martin Ngoga, ambaye ni Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Rwanda alipozungumza kwa simu kutoka Kigali jana.

Aliliambia shirika la habari la Hirondelle, kwamba hatua hiyo kwa kweli si mahali pake na inaweza kabisa kudhalilisha hadhi ya Mahakama za Umoja wa Mataifa. Rwanda hairuhusu sera ya aina hiyo.

Hasira hizo zilitolewa kutokana na tangazo la wiki iliyopita, kwamba kuanzia Mei mwaka huu Mahakama hiyo ilibadilisha sera yake, ili kuruhusu watuhumiwa na wafungwa kutembelewa na wenzi wao na kujamiiana.

Baadhi ya nchi zinaamini kuwa mfungwa hawezi kupewa haki ya starehe ya kujamiiana, hata kama anayefanya naye hivyo ni mkewe kisheria, wakati akitumikia kifungo kama sehemu ya adhabu.

Lakini kwa upande mwingine, wana harakati wa haki za binadamu wanatetea kuwa hata kama mtu amefungwa, ana haki ya kushiriki na familia yake.

Nchi wahafidhina kama vile Saudi Arabia, zimeruhusu matembezi kama hayo kwa miaka kadhaa sasa, lakini nchi kama Uingereza, Uskochi na Ayalandi haziruhusu.

Nchini Brazili, wafungwa wa kiume wanaruhusiwa kutembelewa na wake zao, wakati kwa wanawake matembezi hayo yanadhibitiwa.
.............................